KIUNGO mkabaji wa kimataifa, Taddeo Lwanga na Francis Kahata majina yao yameondolewa kwenye orodha ya wachezaji wa Simba watakaocheza Ligi Kuu Tanzania Bara kuanzia mzunguko wa pili unaotarajiwa kuanza Februari 19.
Lwanga aliyesajiliwa dirisha dogo lililofungwa Januari 15 na Kahata watakuwa wakicheza mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika pekee baada ya Simba kusajili wachezaji 12 wa kimataifa.
Katika orodha ya usajili iliyotolewa na Shirikisho la Soka (TFF), Perfect Chikwende aliyesajiliwa siku ya mwisho ya dirisha dogo la usajili akitokea FC Platinum ya Zimbabwe na Doxa Gikanji kutoka DC Motema Pembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo watakuwa wakicheza Ligi Kuu Tanzania Bara pekee.
Simba imesajili wachezaji 12 wa kimataifa wakati kanuni za ligi zimeweka wazi kikomo mwisho wachezaji 10 ndio maana Kahata na Lwanga majina yao yakaondolewa kwenye ligi.
Hata hivyo, Chikwende asingeweza kucheza Ligi ya Mabingwa Afrika kwa sababu kanuni za Caf zinasema mchezaji mmoja hawezi kucheza timu mbili tofouti ndani ya mashindano hayohayo.
Simba ilifuzu hatua ya makundi baada ya kuifunga FC Platinum kwa jumla ya mabao 4-1.
Wakati huo huo, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limevitaka vilabu kufanya marekebisho ya uhakiki wa makosa kwa wachezaji walioombewa usajili kwani kama yatakuwa na mapungufu kikanuni hayatapatiwa uthibitisho wa usajili hivyo hawatapata leseni