Rostenburg. Kocha wa Simba, Patrick Aussems amesema alipenda kuendelea kufanya kazi na Emmanuel Okwi raia wa Uganda na Mghana James Kotei, lakini wachezaji hao wameondoka.
Alisema hajui sababu za wachezaji hao kutoongeza mkataba, lakini anafikiri huenda walipata timu zilizowapa dau kubwa ndiyo sababu ya wao kuondoka.
Aussems alisema, taarifa za kuondoka kwao zilimshtukiza lakini kwa sababu mpira ni maisha yao, hakuwa na namna ya kuwazuia.
“Okwi na Kotei hawakuwa miongoni mwa wachezaji saba walioachwa, sikupendekeza wachezaji hao kuondoka lakini wamefanya hivyo kutafuta maisha, “alisema Aussems.
“Wenyewe waliniambia kuwa wamepata ofa kubwa ndio maana waliamua kuondoka, nikasema sawa.” alisema
Alisema alikubali matokeo kwa kuwa kocha anaweza kupendekeza mchezaji lakini mwenyewe akawa hayuko tayari kuwepo katika kikosi
Pia Soma
- Ratiba ya CAF: Simba kwa UD Songo, Yanga yatupwa kwa Rollers
- Azam FC kutetea ubingwa Kagame leo
- Kilichoibeba Algeria Afcon
Wachezaji ambao wameondoka na Okwi, Kotei ni Juuko Murshidi, (Uganda) Haruna Niyonzima (Rwanda), Asante Kwasi na Nicholas Gyan (Ghana) na Zana Coulibaly raia wa Ivory Coast.
Simba imeweka kambi nchini hapa kujiandaa na mashindano ya Ligi Kuu Tanzania Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika.
Simba ndio mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara waliotwaa msimu uliopita.