KOCHA Msaidizi wa kikosi cha KMC, Habibu Kondo amesema Yanga wasitarajie mteremko katika mchezo wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaochezwa mwishoni mwa wiki hii kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
KMC imekuwa kwenye kiwango bora msimu huu katika Ligi Kuu ikishinda michezo 10 kati ya 24 iliyocheza na inashika nafasi ya tano kwenye msimamo wa ligi inayoshirikisha timu 18.
Akizungumza Dar es Salaam jana baada ya mazoezi ya timu hiyo yaliyofanyika Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam, Kondo alisema wanaendelea kujiandaa kwa ajili ya mchezo dhidi ya Yanga na mechi za Kombe la Shirikisho la Azam.
“Kikosi kinaendelea na maandalizi ya mechi yetu na Yanga na mechi za Kombe la Shirikisho la Azam, malengo yetu ni kufanya vizuri kwenye mechi zetu zote zilizobakia ili tuweze kumaliza nafasi za juu katika msimamo wa ligi.”
“Ushindani kwenye ligi umeongezeka ikizingatiwa kila timu inapambana kumaliza kwenye nafasi nzuri, hivyo ni lazima tufanye maandalizi ya kutosha ili kufanya vizuri kwenye kila mechi ,” alisema.
Mchezo wa mzunguko wa kwanza uliozikutanisha timu hizo jijini Mwanza katika Uwanja wa CCM Kirumba, KMC FC waliokua wenyeji walifungwa mabao 2-1.