Baada ya klabu ya KMC kuachana na aliyekuwa kinara wa mabao msimu uliopita, Matheo Anthony leo imekamilisha usajili wa Ibrahim Elius raia wa Kenya mwenye asili ya Somalia.
KMC wamekamilisha dili hilo kwa mkataba wa miaka miwili kutoka klabu ya Kibra United inayoshiriki Ligi Kuu Kenya na tayari ametangazwa.
Chanzo cha habari kutoka ndani ya KMC kilisema kuwa huo ni usajili wa mwisho kwao na tayari mchezaji huyo amejiunga na timu yao iliyopo kambini Zanzibar.
“Usajili umeshakamilika na mchezaji huyo amejiunga tayari, tumemaliza usajili kilichobaki ni maandalizi tu kwasasa, tuna imani kubwa naye tunaamini ataongeza nguvu eneo la ushambuliaji;
“Tumefanya usajili ambao tunaamini utakuwa na chachu ya ushindani msimu ujao lengo ni kuona tunakuwa bora na kuonyesha ushindani kwa wapinzani wetu hatutaki kurudia makosa ya msimu uliopita kwa kuwa miongoni mwa timu zitakazocheza playoff.” kilisema chanzo hicho
Alipotafutwa Mkurugenzi wa KMC, Daniele Mwakasungula kuzungumzia usajili wao alisema; "Taarifa zote za usajili unapokamilika zinawekwa wazi."