Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Job aanika siri za ushindi wa Geita Gold

Dickson Job Yanga Xd Job aanika siri za ushindi wa Geita Gold

Fri, 15 Mar 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Beki na nahodha msaidizi wa Yanga, Dickson Job amesema ushindi wa bao 1-0 iliyoupata dhidi ya Geita Gold jana usiku si haba kutokana na mchezo huo kuwa na presha kwenye safu ya beki na wapinzani wao walicharuka hasa kipindi cha pili, kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi.

Job amesema wanachofurahia ni kupata pointi tatu muhimu zinazowafanya waendelee kuongoza msimamo wa Ligi Kuu Bara, huku pia wakiendeleza 'clean sheet' kwenye safu yao ya beki na zaidi akimmwagia sifa kipa Djigui Diarra kwa alivyosahihisha makosa ya mabeki na wakati mwingine kuwa mkali, lengo likiwa ni kuhakikisha wanatoka salama kwenye pambano hilo.

Beki huyo huwa wanafuraha wakiwafunga wapinzani wao kuanzia mabao matatu na kuendelea kwani kama mabeki inawasaidia kucheza kwa kujiamini tofauti na wakifunga bao moja.

“Kuifunga timu pinzani kuanzia mabao matatu na kuendelea sio kuionea, wanastahili, kuna msemo kila mmoja atavuna alichopanda, hivyo wakifungwa mabao mengi wamevuna walichopanda na sisi tunacheza kwa uhuru,” amesema Job na kuongeza;

“Timu ikiwa imefunga bao moja mabeki tunacheza kwa presha kitu ambacho kwenye soka sio sahihi, hivyo hakuna kipindi tunakuwa na raha uwanjani kama timu inaongoza mabao matatu na kuendelea, ugumu unakuwa ni pale tuna bao moja na wapinzani wanatafuta matokeo.”

Akizungumzia namna wanavyofanya kazi na Diarra ambaye amekiri ni mkali zaidi akiwa langoni amesema anamwelewa na huwa hata wao wanachukulia kama sehemu ya kazi, hivyo wanajitahidi kupunguza makosa na kucheza kwa kuelekezana.

“Diarra kweli anatufokea, lakini ni sehemu ya kazi, huwa hatuchukulii kama tatizo na ndio maana unaona timu inafanya vizuri na kitu ambacho wengi hawafahamu sio kipa tu anakuwa mkali wachezaji wote uwanjani ukikosea wanakwambia ukweli,” amesema Job na kuongeza;

“Yanga hakuna mkongwe wala mdogo, ukikosea unaambiwa ukweli na baada ya mchezo maisha mengine yanaendelea, hakuna ambaye anachukia kuambiwa ukweli, kila mmoja anataka mafanikio na kujifunza hivyo tunaelekezana.”

Amesema ili wapate ushindi mabeki hawatakiwi kuruhusu bao kabla ya timu haijafunga, jambo ambalo linahitaji kujituma na kuwa na maelewano mazuri kuanzia kipa na wao wenyewe.

“Jukumu letu sisi kama mabeki ni kukaba kwa asilimia zote ili tusiweze kuruhusu bao na kuwapa nguvu washambuliaji wetu ambao kwa namna moja ama nyingine wanatupa nguvu za kujiamini kutokana na kazi nzuri wanayoifanya wamekuwa bora sana eneo hilo sitaki kumtaja mchezaji mmoja mmoja lakini wamekuwa imara sana,” amesema.

Yanga ilipata ushindi huo ukiwa ni wa 17 kwa msimu huu katika ligi kati ya mechi 19 iliyocheza na kufikisha pointi 52 zilizozidi kuiweka pazuri kwenye mbio za kutetea ubingwa huo inaoushikilia kwa msimu wa pili mfululizo kwa sasa.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live