Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ivory Coast imetibua ujanja wa Pacome

Pacome Ivorys Ivory Coast imetibua ujanja wa Pacome

Fri, 22 Mar 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Dakika 90 za mechi baina ya Azam na Yanga zikamalizika kwa Matajiri wa jiji kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Wananchi na furaha zaidi ushindi huo ulipatikana huku wakiwa wametoka kutanguliwa.

Ilikuwa ni habari ya kuvutia kwa Azam kwani kabla ya hapo walikuwa wamefungwa mechi tano mfululizo na Yanga hivyo ushindi huo ulikuwa kwa kiasi kikubwa umewafanya wapooze machungu.

Kana kwamba haitoshi, matokeo hayo yakasaidia kuweka hai matumaini yao ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu msimu huu na sio wao peke yao bali hata kwa Simba iliyopo nafasi ya tatu.

Maana kama Azam ingepoteza mechi hiyo, ndoto za ubingwa ni kama zingekufa tu rasmi kwa vile wangeachwa kwa tofauti ya pointi nane na wakati huo Yanga ingebaki na faida ya mechi moja mkononi.

Matokeo kwa Yanga yaliwaumiza lakini kubwa zaidi ambalo liliwapa hofu ni kushindwa kuendelea na mchezo kwa nyota wake Pacome Zouzoua kwa kile kilichoonekana amepata majeraha.

Hata hivyo, kwa wasomi wa Cuba tukaelewa kilichofanyika pale ni kucheza na akili za mpinzani ajaye kwenye hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, Mamelodi Sundowns na kuwaingiza mkenge.

Si unajua tena jamaa wameshatuma mashushushu wao wapo hapa nchini hivyo Yanga inajitahidi kucheza na akili zao na inaonekana mojawapo ikawa hiyo ya majeraha ya kiandamizi ya Pacome Zouzoua labda kuwahadaa Masandawana.

Hata hivyo, ndani ya muda mfupi tu, pepa limevuja baada ya Ivory Coast kumwita ghafla Pacome na nyota huyo kujiunga na kambi ya timu yao ya taifa huko Ufaransa kwa ajili ya michezo ya kirafiki.

Kuitwa kwa Pacome na kwenda maana yake kunaishtua Mamelodi kuwa hakuna majeraha yatakayomfanya mchezaji huyo aikose mechi dhidi yao hivyo wataendelea kujiandaa kumdhibiti.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live