Wakati taarifa zikienea kwamba tiketi za mchezo wa kwanza wa Taifa Stars dhidi ya Morocco zimemalizwa na Waarabu hao umetolewa ufafanuzi.
Makamu wa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Athuman Nyamlani amesema wamelazimika kwenda kutafuta usahihi wa taarifa hizo na kukutana na taarifa tofauti.
Nyamlani amesema tiketi hizo zimenunuliwa na mashabiki tofauti ambao watakwenda kutazama mechi zote mbili za leo zinazochezwa kwenye Uwanja mmoja ndani ya Jiji la San Pedro.
"Unajua leo mechi zote mbili zinachezwa hapa ndani ya mji huu wa San Pedro kwahiyo hapa leo ni kama mtoko wa mji huu ," amesema Nyamlani.
"Ukiacha wenyeji pia Mataifa yote manne DR Congo, Zambia, Morocco na sisi Tanzania na watu wengine nao wamekuwa wakizinunua hizi tiketi ya mechi hizi.
"Bahati mbaya mchezo wetu ni wa kwanza kwahiyo hapo ndipo uhaba wa tiketi ulipokuja labda inawezekana kwamba mashabiki wa Morocco wakawa wengi kuliko wengine ingawa halina uhakika mpaka sasa, kama haukununua mapema kidogo utapata shida.
Baada ya mechi ya Stars dhidi ya Morocco utakaoanza saa 2:00 usiku Uwanja huo huo utatumika kwenye mchezo kati ya Zambia na DR Congo utakaoanza saa 5:00 usiku
Akizungumzia maandalizi ya kikosi cha Taifa Stars Nyamlani amesema kila kitu kipo sawa na kwamba kikosi kinasubiri muda wa mchezo kwenda kulipigania Taifa.
"Watanzania walioko huko nyumbani waendelee kuwaombea vijana wao, sisi tuliopo hapa tumejirodhisha kila kitu kipo sawa na wachezaji wanasubiri muda wa mchezo tu wakafanye kazi."