Kocha Mkuu wa Simba, Hitimana Thierry, amewataka nyota wote wa kikosi hicho ambao hawana majukumu timu za taifa kuripoti kambini kuanzia kesho Jumatatu kwa ajili ya kusuka upya mikakati ya kutetea ubingwa msimu huu.
Licha ya kuanza kwa kusuasua msimu huu, Simba inakamatia nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara ambapo imefanikiwa kukusanya pointi 11 katika michezo mitano, wakishinda mitatu na sare mbili. Inazidiwa na vinara Yanga kwa pointi nne.
Akizungumza, Mkuu wa Maudhui wa Simba, Ally Shatry, alisema: “Baada ya kuwa na mapumziko ya muda mfupi kufuatia ratiba ya mashindano ya timu za taifa, tunatarajia kikosi kitarejea kambini Jumatatu kwa ajili ya kuanza kujiandaa na mchezo ujao wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Ruvu Shooting utakaochezwa Novemba 19, mwaka huu kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.”
Naye Hitimana akizungumza na Spoti Xtra kuhusu mipango yake, alisema: “Tuna kikosi bora ambacho bila shaka kinaweza kutetea ubingwa wetu msimu huu licha ya kuwa na mwanzo mgumu, lakini tumepanga kutumia muda huu wa mapumziko katika kuhakikisha tunafanyia mapungufu tuliyoonesha katika michezo mitano iliyopita.”