Baada ya sare ya 1-1 katika mechi ya kwanza ya Kariakoo Derby kwenye Ligi Kuu Bara msimu huu, miamba Simba na Yanga itarudiana tena ili kumaliza ubishi baina yao katika pambano litakalopigwa Aprili 16 mwaka huu katika uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Presha na kasi kubwa katika mechi ya watani hao ni vitu vinavyowafanya wachezaji wa klabu hizo kushindwa kudumisha nidhamu ya mchezo kwa dakika 90 na matokeo yake wamekuwa wakipata kadi nyekundu ingawa wakati mwingine lawama zimekuwa zikitupwa kwa waamuzi.
Katika mechi yao ya kwanza, Simba ilitangulia kwa bao la Augustine Okrah kabla ya Stephane Aziz KI kusawazisha sekunde chache kabla ya mapumziko ya mechi hiyo iliyopigwa Oktoba 23.
Mechi hiyo ya watani itakuwa ni ya kwanza kwa kocha wa Simba,Roberto Oliveira ‘Robertinho’ akiwa na timu hiyo,huku ikumbukwe kocha huyo amewahi kukutana na Yanga mechi ya kirafiki katika kilele cha wiki ya Mwananchi alipokuwa akiinoa Vipers ya Uganda na kuwafunga wenyeji kwa mabao 2-0.
Wachezaji wafuatao wanaweza kupata kadi nyekundu kutokana na aina ya uchezaji pamoja na pressure ya mechi.
SADIO KANOUTE Mwamba huyu raia wa Mali ambaye Simba ilimsajili kutokea timu ya Al Ahli Benghazi ya nchini Libya amekuwa na kiwango bora msimu huu.
Kanoute amepewa kadi moja nyekundu katika Ligi Kuu Bara na aliipata katika mchezo dhidi ya Coastal Union Desemba 3 mwaka jana na alipewa na mwamuzi Jonesia Rukyaa.
Aina ya uchezaji wake umekuwa ukimfanya apate kadi nyingi za njano na mara nyingine nyekundu.
Kuelekea katika derby hiyo mwanaspoti inaona kuna uwezekana wa mchezaji huyo kupata kadi nyekundu kwani viungo wa Yanga wengi ni wachezaji wenye uwezo wa kumiliki mpira kama Khalid Aucho Abubakari Salum ‘Sure Boy’,Kenned Musonda Pia Yanga ina wachezaji wenye kasi kama Benard Morrison,Farid Musa,Tuisila Kisinda na Jesus Muloko.
JONAS MKUDE Mkude amepoteza namba katika kikosi cha Simba lakini bado anaweza kupata nafasi ya kucheza kwani katika mchezo wa mwisho wa Ligi Kuu dhidi ya Ihefu alikuwepo kwenye benchi.
Mkude miongoni mwa wachezaji wanaoingia kwenye orodha ya wachezaji waliotolewa nje ya uwanja kwa kadi nyekundu katika mchezo wa watani wa jadi Oktoba mosi 2016.
Alionyeshwa kadi nyekundu ya moja kwa moja dakika ya 26 ya kipindi cha kwanza baada ya kumsukuma mwamuzi.
Kiungo huyo wa Simba alifanya kitendo hicho baada ya mwamuzi wa mchezo huo kulikubali bao lililofungwa na mshambuliaji wa Yanga, Amiss Tambwe, ambae alifunga kutokana na kuukontroo mpira kwa kutumia mkono wake wa kulia, licha ya Simba kuwa pungufu mchezo huo ulimalizika kwa sare ya bao 1-1.
Uchezaji wake wa kupambania mipira inayodondoka inaweza kumfanya akapa kadi nyekundu katika mchezo huo kama kocha atampa nafasi ya kucheza.
MZAMIRU YASSIN Ni mara chache sana kumaliza dakika 90 bila ya kuwa na kadi ya njano,kutokana na aina ya uchezaji wake.
Ukabaji wake wa kuipunguza timu pinzani makali unamweka katika hatari ya kupata kadi nyekundu kutokana na kucheza faulo nyingi.
Mzamiru amejihakikishia namba katika kikosi cha Kocha Roberto Robertinho kutokana na uwezo wake wa kukaba.
BACCA NA MWAMNYETO Kutokana na uwezo unaooneshwa na mshambuliaji wa Simba,Jean Baleke kuna uwezekano mabeki wa Yanga wakampania mshambuliaji huyo.
Mmoja ya mabeki hao ambao watapewa kazi ya kumlinda Baleke ni Ibrahim Bacca na Bakari Mwamnyeto ambao aina ya uchezaji wao unaweza kusababisha upatikanaji wa kadi nyekundu ama ya pili ya njano.
Bacca msimu huu amekuwa na kiwango bora akimnyanganya namba Dickson Job ambaye wakati mwingine amekuwa akipangwa namba 2 huku Mwamnyeto akijihakikishia namba kutokana na ukabaji wake na utulivu anapokuwa na mali.
AUCHO Mchezo huo utaamuliwa na viungo siku hiyo amini ninachokwambia hivyo kutakuwa na ‘bato’ la hatari hasa katikati ya uwanja kati ya Mzamiru, Kanoute kwa Simba na Khalid Aucho na Mudathir Yahaya kwa Yanga.
Aucho amekuwa akigongana sana na pia ni mchezaji anayeonekana wakati mwingine kucheza akiwa amepaniki, hivyo kuna uwezekano wa kuweza kupata kuanzia ya njano hadi ile kadi nyekundu kama atatuliza akili uwanjani.
MUDATHIR YAHAYA Utasema nini kwa huyu mchezaji ambaye amegeuka kuwa kipenzi cha mashabiki wa Yanga kutokana na aina ya uchezaji wake pamoja na kuhakikisha timu inakuwa salama.
Mchezaji huyo ni kama amezipa pengo la Feisal Salum na amekuwa akitekeleza kwa ufasaha maelekezo ya benchi la ufundi la Yanga linaloongozwa Nasredin Nabi.
INONGA Henock Inonga atataka kumdhibiti Fiston Mayele wa Yanga ili asifunge katika mchezo huo na kila mmoja anajua vita ya wachezaji hao.
Kule kupaniana kunaweza kusababisha Inonga akapata kadi nyekundu katika mchezo huo kwani Mayele amekuwa hashikiki msimu huu ameishaweka kambani mabao 15.