HUKO Ligi Daraja la Kwanza (FDL) unaambiwa hatumwi mtoto sokoni kwani ligi hiyo inaelekea ukingoni huku kila timu ikitaka kumaliza ikiwa katika sehemu salama.
Ukiachana na mbio za kuwania kupanda daraja na kukwepa kushuka daraja, moto mwingine unawashwa kwenye kuwania tuzo ya mfungaji bora ambapo mastaa wengi wanaisaka kwa udi na uvumba.
Kutoka kundi A ambapo kila timu imemabakiza mechi mbili pekee kumaliza ligi, chati ya wafungaji inaongozwa na William Mwampangama wa Mbeya Kwanza mwenye mabao tisa, akifuatia John Mahundo wa Mawenzi Market mwenye bao nane.
Wengine ni Emmanuel Mkoba na Adam Uledi wa African Sports wote wenye bao sita kwa kila mmoja sambamba na Lucas Sendama wa Ken Gold na Oscar wenye bao sita huku Mwansanga wa Mbeya Kwanza na Barnaba Mlomo wa Njombe Mji kila mmoja akiwa na bao nne.
Katika kundi B ambapo baadhi ya timu zimebakiza mechi nne na nyingine tano, chati ya wafumania nyavu inaongozwa na Offen Chikola wa Fountain Gate na Venance Ludovic wa Geita Gold kila mmoja akiwa na bao nane.
Wengine ni Emmanuel Haule wa Pamba mwenye bao tano huku chini yake wakiwepo Selemani Abdallah wa Rhino Rangers, Athumani Kisatu na Iddi Mbaga wote wa Transit Camp kila mmoja akiwa na bao nne.