Beki wa kimataifa wa Tanzania, Haji Mnoga aliyefanya vizuri kwenye michezo miwili mfululizo ya timui ya taifa, Taifa Stara kuwania Fainali za Kombe la Dunia 2026, ameanza kuona mwanga kikosini na kumtaja kocha Adel Amrouche kuwa nyuma ya kiwango alichokionyesha hadi sasa katika timu hiyo.
Haji aliyerejea Ulaya kuendelea na majukumu ya klabu anayoichezea ya Aldershot Town akicheza kwa mkopo akitokea Portsmouth, alifichua hilo jana alipozungumza na Mwanaspoti na kusema akidai utofauti wa mazingira ulikuwa ukimtatiza kabla kuzoea, ikumbukwe kuwa beki huyo amezaliwa na kukulia England.
Beki huyo Mzanzibar, alisema; “Ukiwa unacheza Ulaya ni wazi, watu watataka kuona utofauti wako, mwanzoni nilikuwa nikipambana kuzoeana na wachezaji wenzangu hata mazingira nayo, namshukuru sana kocha (Adel) kwa imani ambayo amekuwa nayo kwangu na pia nawashukuru sana Watanzania kwa upendo wao.”
“Mi ni mapambanaji, sipendi kuona timu ikipoteza, ndio maana nimekuwa nikijitoa na bado najiona kuwa na nafasi ya kufanya zaidi, hivyo tukutane fainali za Afrika.”