Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Haaland awaacha mashabiki mdomo wazi

Haaland X Ronaldo Haaland awaacha mashabiki mdomo wazi

Thu, 15 Feb 2024 Chanzo: Mwanaspoti

Straika la mabao, Erling Haaland amewaacha vinywa wazi mashabiki baada ya kuruka futi 7 na inchi 6 wakati Manchester City ilipokipiga na FC Copenhagen katika mchezo wa kwanza wa hatua ya 16 bora kwenye mtoano wa Ligi ya Mabingwa Ulaya usiku wa Jumanne.

Straika huyo mwenye kimo cha futi 6 na inchi 4 alipangwa kwenye kipute hicho cha Ligi ya Mabingwa Ulaya kuwakabili miamba hiyo ya Denmark.

Haaland, 23, hakufunga kwenye mchezo huo na kikosi chake cha Man City kiliibuka na ushindi wa mabao 3-1 na hivyo kujiweka pazuri kabla ya mechi ya marudiano itakayofanyika mwezi ujao huko Etihad.

Lakini, bado alifanya kitu kilichowafanya mashabiki kupata kitu cha kuzungumza. Staa huyo aliruka juu kuunganisha mpira wa krosi, lakini kilichovutia ni kitendo chake cha kuruka hewani futi 7 na inchi 6.

Aliupata mpira, lakini hakuweza kulenga goli, kitu ambacho kama angefunga, basi bila shaka lingekuwa moja ya mabao bora kabisa kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu huu.

Tukio hilo la Haaland lililinganishwa na lile la Cristiano Ronaldo, wakati alipokuwa akikipiga Real Madrid na kuwafunga bao Juventus katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya mwaka 2018.

Kwenye tukio la Ronaldo, supastaa huyo wa Ureno aliruka hewani futi 7 na inchi 8, kuunganisha krosi ya beki Dani Carvajal na kuusukuma mpira kwenye nyavu za Juventus, tukio ambalo liliwafanya mashabiki uwanja mzima kusimama kushangilia bao tamu bila ya kujali aliyefungwa.

Ronaldo alipigiwa makofi na mashabiki wa Juventus, timu ambayo alikwenda kujiunga nayo baadaye mwaka huo, na Mreno huyo anayekipiga Al-Nassr kwa sasa, akizungumzia bao lake alisema: “Lilikuwa tukio matata kabisa. Nawashukuru sana walioshangilia, mashabiki wote wa Juventus.

“Walichofanya kunishangilia kilikuwa safi, nimefurahi sana. Nawashukuru sana, hiki kitu kilikuwa hakijawahi kwenye maisha yangu.”

Katika mchezo huo wa usiku wa Jumanne, straika Haaland aliambiwa na kocha wake Pep Guardiola acheze tu kwa utulivu. Hakufunga bao, lakini mashabiki wa Man City walifurahishwa na jaribio lake la kutaka kufunga kwa tick-tack bao matata kabisa. Shabiki mmoja aliandika kwenye mtandao wa kijamii: “Ile inawezekanaje?”

Mwingine alisema: “Kaka alikuwa na ubora mkubwa.”

Shabiki wa tatu alisema: “Alikuwa anaelea.”

Shabiki mwingine aliongeza: “Yupo kwenye ligi yake mwenyewe.”

Haaland amefunga mabao 73 katika mechi 79 tangu alipojiunga na Man City akitokea Borussia Dortmund dirisha lililopita la uhamisho wa majira ya kiangazi.

Ndiye kinara wa mabao kwenye Ligi Kuu England msimu huu akifunga mabao 16, licha ya kwamba alikosa miezi miwili kutokana na kuwa majeruhi.

Chanzo: Mwanaspoti