Miguel Gutierrez amewashangaza Barcelona kwa bao zuri na kuipa Girona bao la kuongoza kwa mara ya pili kipindi cha kwanza cha kusisimua katika mechi ya LaLiga.
Girona ilipata bao la mapema lililowekwa kimiani na Artem Dovbyk kabla ya Gutierrez kufunga bao la pili, Barcelona ikiwa nyuma kwa bao 1-0 kabla ya Robert Lewandowski kusawazisha dakika ya 19.
Girona imekuwa hatari msimu huu wa LaLiga mpaka sasa, imeendeelea kuonyesha ubabe kwenye ligi kwa kuifunga Barcelona mabao 4-2 kwenye Uwanja wa Olympic.
Ushindi wa Girona unakuwa wa 13 katika mechi 16 kwenye ligi, huku ikiishusha Real Madrid kileleni kwenye msimamo wa LaLiga baada ya kuambulia sare ya bao 1-1 dhidi ya Real Betis.
Pia, kikosi cha Kocha Michel hakijapoteza mechi tangu kilipofungwa mabao 3-0 na Madrid Septemba na imekuwa imara zaidi baada ya kichapo hicho.
Bingwa mtetezi imeshindwa kujitetea mpaka sasa huku maswali yakiulizwa kuhusu kibarua cha Kocha Xavi Hernandez kutokana na kiwango cha msimu huu.
Kutokana na kipigo hicho Barcelona imeendelea kubaki nafasi ya nne kwa tofauti ya pointi saba dhidi ya Girona.
Barca itacheza mechi ya mwisho ya hatua ya makundi ya Ligi Mabingwa Ulaya dhidi ya Antwerp kesho kabla ya mechi ya LaLiga dhidi ya Valencia. Baada ya mtanange huo, itamenyana na Almeria kabla ya mapumziko.