Baada ya kuruhusu bao 1-0 ugenini dhidi ya Hilal Alsahil SC ya Sudan kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika, kocha Fred Felix ‘Minziro’ amesema anaona mwanga mzuri kwenye mechi ya marudiano.
Geita itawakaribisha wapinzani wao kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam, Septemba 17 mwaka huu. “Timu ilitengeneza nafasi nyingi lakini ilishindwa kutumia, naamini ningekuwa na mshambuliaji wangu asili kuna kitu kingefanyika,” alisema na kuongeza;
“Nimewasoma wapinzani wangu nafahamu ubora wao uko eneo gani na udhaifu wao, nina kazi kubwa ya kufanya kwenye uwanja wa nyumbani ili kutengeneza timu imara zaidi ambayo itamaliza mchezo nyumbani,” alisema.
Minziro alisema anatarajia mchezo mzuri kutoka kwa wachezaji wake kwenye mechi ya marudiano huku akisisitiza kuwa eneo la ushambuliaji linatakiwa kuwa na maboresho ili kutumia kila nafasi itakayotengenezwa.