Mchezo wa Ligi kuu ya NBC wa Geita Gold dhidi ya Yanga umezidi kupamba moto huku uongozi wa Wachimba Dhahabu ukichimba mkwara kuwa tambo za Yanga kutopoteza mchezo wa ligi zitakoma Jumamosi.
Mchezo huo utapigwa keshokutwa Jumamosi saa 10 jioni katika Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza viingilio vikiwa Sh 20,000 (jukwaa kuu), Sh 10,000 (jukwaa la kawaida) na sh 5,000 mzunguko huku Yanga ikiwa na kumbukumbu na kuifunga Geita Gold katika uwanja huo msimu uliopita.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari jijini hapa, Kaimu Katibu Mkuu wa Geita Gold, Liberatus Pastory amesema maandalizi ya mchezo huo yamekamilika huku akisema kikosi chao kimeshatia nanga jijini Mwanza baada ya mchezo wa Ligi jana (juzi) ugenini dhidi ya Ruvu Shooting na leo (jana) wachezaji wamepewa mapumziko.
"Tumejiandaa kwa mchezo huu, tuna uhakika tutakuwa na mchezo mzuri na kupata matokeo kama ambavyo imekuwa katika Mechi zetu nne zilizopita, tuna imani sisi ndiyo tutasitisha rekodi ya Yanga kutofungwa kwenye ligi wachezaji waendelee kujituma kwa spirit na nguvu ile ili tuweze kutimiza malengo yetu," amesema Kaimu Katibu Mkuu wa Geita Gold, Liberatus Pastory
Kwa upande wake, Katibu Msaidizi wa Chama cha Soka Mkoa wa Mwanza (MZFA), Khalid Bitebo ameipongeza Geita Gold kwa kuuleta mchezo huo jijini hapa huku akiwatoa hofu mashabiki wa soka wanaotarajia kwenda kuushuhudia mchezo huo kuwa ulinzi umeimarishwa na watapata burudani ya kutosha bila kubughudhiwa.