Kocha Mkuu wa Yanga, Miguel Gamondi amesema kuwa ukame wa mabao mengi unasababishwa na ugumu wa ligi katika mechi hizi kuelekea mwisho wa msimu ambapo kila timu inataka matokeo chanya ili kujihakikishia nafasi nzuri.
Gamondi ambaye timu yake msimu huu imesifika kugawa kipigo cha bao tano tano amesema hayo kuelekea mchezo wa kesho wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya Kagera ambapo amedai kuwa utakuwa mchezo mgumu hasa ikikumbukwa kuwa Kagera ndiyo timu ya kwanza msimu huu kutoa sare na Yanga katika mzunguko wa kwanza.
“Kama mnavyofahamu tulifika jana kutoka Kigoma, tutafanya mazoezi leo. Tumefanya uchambuzi wetu kuhusu Kagera Sugar na leo tutakamilisha kila kitu kuhusu mchezo ujao.
“Tunajua mchezo wa kesho utakuwa mgumu na sio dhidi ya Kagera Sugar tu lakini timu zote michezo imekuwa migumu kuelekea mwisho wa msimu kwani kwa sasa kila mmoja anataka nafasi nzuri.
“Kama mmetazama mechi tano za mwisho zimekuwa ngumu, na ukiangalia hakuna mabao mengi yanayofungwa, ni mabao machache sana kwa mechi.
“Kagera wana timu nzuri na walitupa changamoto sana kwao kwenye mchezo wa kwanza lakini kesho tutakuwa nyumbani Chamazi, nategema utakuwa mchezo mgumu pia kwa sababu hata Kagera wana matumaini ya kupata alama tatu kutoka kwa Yanga,” amesema Gamondi.