Kocha Mkuu Yanga SC, Miguel Gamondi amesema kuwa yeye benchi lake na Ufundi pamoja na wachezaji wake watapambana kufa na kupona katika mechi zilizosalia za Ligi ya mabingwa Afrika hatua ya Makundi ili kuhakikisha kuwa wanatoboa kwenda robo fainali.
Gamondi amesema hayo mara baada ya kurejea dar es Salaam na kikosi chake akitokea Kumasi nchini Ghana ambako Yanga ilikwenda kuchewza na Medeama FC na kutoa sare ya bao 1-1.
“Najua alama tulizonazo, hilo linanisumbua, lakini naiamini timu yangu, naamini kwenye soka kila kitu kinawezekana, wakati unawakilisha timu kubwa kama Yanga Afrika unatakiwa kupambana kwa kila kitu, unatakiwa kucheza hata pale unapojua kwamba ni ngumu kuingia hatua inayofuata, nawaahidi tutapambana mpaka mwisho,” amesema Miguel Gamondi.
Yanga inashika mkia kwenye kundi lake ikiwa na alama 2 tu ambapo imetoa sare 2 na kufungwa moja huku Al Ahly wakiongoza kundi na alama 5. CR Belouizdad na Medeama wote wana alama nne kila mmoja.
Mchezo ujao Yanga itarudiana na Medeama katika Dimba la Mkapa kabla ya kuwakaribisha Belouizdad na mchezo wa mwisho utakuwa ugenini dhidi ya Al Ahly.