Jana, Julai 10, 2023, kikosi cha Yanga kimeanza kuripoti kwenye kambi yao iliyopo Avic Town, Kimbiji Jijini Dar es Salaam, kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya.
Uongozi wa Klabu hiyo ulitangaza mapema kuwa, kutokana na muda wa kujiandaa kuwa mchache, hivyo timu itaweka kambi hapa hapa Tanzania na hakutakuwa na safari ya kwenda nje ya nchi.
Uamuzi huo umepokelewa vyema na kocha mkuu Angel Miguel Gamondi ambaye ameanza kupanga silaha nzito kuelekea mechi ya kilele cha Wiki ya Wananchi na zile za Ngao ya Hisani.
Gamondi tayari ameshapanga ratiba nzima ya ‘Pre Season’ baada ya kufanya kikao kirefu na meneja wa timu, Walter Harrison.
Akizungumza na Yanga Media, Gamondi alisema, ”Hakuna muda wa kuchelewa zaidi. Wachezaji wameshaanza kuripoti kambini na kazi kubwa iliyokuwa mbele yetu ni kutengeneza timu nzuri ya kwenda kushindana msimu ujao.”