Beki wa Singida Big Stars, Gadiel Michael amesema kitendo cha kocha wake kumuamini na kumpa nafasi ya kuanza katika kikosi cha kwanza sio jambo dogo kulingana na alikotoka.
Gadiel ni miongoni mwa wachezaji waliotemwa na Simba baada ya msimu kumalizika, lakni amekuwa lulu katika kikosi hicho cha walima alizeti.
Gadiel amesema kuwa anaamini ubora na ndio maana jicho la viongozi wa timu wakamuona na kumsajili hivyo ni wajibu wake kupambana kuwapa kile walichokihitaji.
“Sisi wachezaji maisha ni popote. Nafurahia uwepo wangu Singida na ni jambo la kumshukuru Mungu kuanza katika kikosi cha kwanza hiyo inaonyesha namna ambavyo kocha ananiamini,” alisema.
Alisema ushindani ni mkubwa na kila mchezaji ana uwezo wa kucheza. Kuhusu mchezo wa juzi kupoteza dhidi ya Azam FC baada ya kufungwa mabao 2-1, alisema ulikuwa mgumu na wenye ushindani lakini bahati iliangukia Azam.
“Tumecheza mpira tumepata nafasi, tumeshindwa kuzitumia na wao wamezitumia ndio mpira tunajipanga mechi bado nyingi tusifanye makosa,” alisema.