Beki wa timu ya wanawake Liverpool, Gilly Flaherty ameweka wazi kuumizwa na yanayoendelea kwenye mitandao ya kijamii ya kumlenga kwa unyanyasaji huku akisema amechukizwa na kitendo hicho na amesema kuwa unyanyasaji huo umefikia kiwango kingine.
Mchezaji huyo wa zamani wa Arsenal, Chelsea na West Ham, ambaye pia aliichezea timu ya Taifa ya Uingereza mapema katika maisha yake ya soka, alihamia Liverpool mwezi Julai.
Flaherty mwenye umri wa miaka 31, amesema kuwa ameshambuliwa sana kwenye mitandao ya kijamii baada ya mechi za Ligi Kuu ya wanawake na mashabiki wa timu yake huku maoni yake kuhusu unyanyasaji huo yakiibua jibu la huruma, na baadhi ya mashabiki wa Liverpool wakisistiza kuwa wakosoaji walikuwa wachache.
Flaherty aliandika kwenye Twitter baada ya Liverpool kupoteza kwa bao 1-0 dhidi ya Tottenham hapo jana huku akisema kuwa; “Kujiunga na timu mpya ni ngumu kwanza lakini kutokubaliwa na mashabiki na kukashifiwa kwenye mitandao ya kijamii baada ya mechi nyingi na mashabiki wako ni kuvunja moyo”.
Beki huyo anaongeza kwa kusema kuwa hajawahi kuwajali mashabiki wa upinzani wanaofanya hivyo lakini wakati mwingine mashabiki hufika kiwango kingine.