Kiungo Mshambuliaji wa Yanga, Feisal Salum ‘Fei Toto’ amewaomba mashabiki wa timu hiyo leo Jumapili kujitokeza kwa wingi katika mchezo wao wa dabi dhidi ya Simba utakaochezwa Uwanja wa Mkapa, Dar.
Fei Toto amesema malengo yao ni kuhakikisha wanaendeleza rekodi ya kuifunga Simba kutokana na ubora wa kikosi chao kwa sasa.
Yanga na Simba zinatarajia kuchezea leo Jumapili katika mchezo wa Ligi Kuu Bara utakaoanza saa 11:00 jioni.
Tangu msimu wa 2021/22, Yanga ikiwa chini ya Kocha Nasreddine Nabi, haijapoteza mchezo wowote dhidi ya Simba wakikutana mara tano katika michuano tofauti, ambapo Yanga imeshinda mechi tatu na sare mbili.
Fei Toto alisema wanajua ugumu na ukubwa wa mchezo huo, lakini amewaomba mashabiki wa timu hiyo kujitokeza kwa wingi kwa kuwa lengo lao ni kuhakikisha wanapata ushindi ili kufikia malengo yao kwenye Ligi Kuu Bara msimu huu.
“Siku zote mechi za dabi huwa ngumu kutokana ukubwa wa mchezo wenyewe, lakini kwa upande wetu tumejipanga na tunatambua umuhimu wa ukubwa wa mchezo wenyewe, tumejipanga kupambana kwa kuhakikisha tunapata ushindi.
“Nadhani jambo kubwa kwetu ni mashabiki kujitokeza kwa wingi katika kutusapoti ili kufikia malengo ya ushindi kwa sababu wapinzani wanatujua na sisi tunawajua vizuri, kitu kikubwa kwa sasa ni sapoti yao ili tupate furaha ya pamoja baada ya dakika tisini,” alisema Fei Toto.