Dar es Salaam. Kocha wa Yanga, Luc Eymael amesema ataishangaza Simba katika mchezo wao wa Jumapili licha ya kuonekana ndio timu bora nchini.
Yanga na Simba zitavaana katika mchezo wa mzunguko wa pili Ligi Kuu Tanzania Bara utakaochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Katika mchezo wa mzunguko wa kwanza timu hizo zilitoka sare mabao 2-2, hivyo mechi ya Jumapili inaweza kuwa na msisimko kwa kuwa kila moja itataka ushindi.
Akizungumza na gazeti hili Dar es Salaam juzi, Eymael alisema Simba ni bora kwa mchezaji mmoja mmoja, lakini haina muunganiko mzuri wa kitimu.
Kocha huyo raia wa Ubelgiji, alisema atatumia udhaifu huo kuishangaza Simba kwa kuwa tayari ana mbinu za kuifunga.
Eymael alisema kwa mtazamo wa wengi Yanga inaonekana ni dhaifu kwa Simba ina rekodi nzuri katika Ligi Kuu msimu huu, lakini hatishiki na rekodi hiyo.
Pia Soma
- Michael Platini aanguka rufaa yake dhidi ya UEFA
- Onyesho la Mariah Carey lapingwa kalenda, kisa corona
- Ronaldinho, kaka yake wakamatwa na paspoti feki Paraguay
“Ni kweli Simba kwa ubora wa mchezaji mmoja mmoja imetuzidi, lakini ukweli ulivyo katika mechi hizi kubwa mara nyingi jambo hilo halipo isipokuwa timu inayocheza kwa pamoja kwa maana ya kushambulia na kukaba kwa nidhamu ndio inafanikiwa,”alisema Eymael.
Kocha huyo alisema wachezaji wako vizuri kisaikolojia na wamejiandaa kuikabili Simba na matumaini yake ni kupata matokeo mazuri kwani hana cha kuhofia.
Eymael alisema ana uzoefu na mechi za watani wa jadi hasa katika soka la Afrika kwa kuwa zinagusa moja kwa moja hisia za mashabiki wa klabu hiyo, hivyo anaipa umuhimu wa pekee.
“Nina uzoefu wa kutosha na mechi kama hizi tangu nikiwa nafundisha Sudan, DR Congo na Kenya. Mchezo huu ili upate matokeo mazuri ni kuandaa mbinu si kuangalia rekodi au matokeo ya nyuma,”alisema.
Yanga ambayo ni mwenyeji wa mchezo huo, inakutana na Simba ikiwa imetokea katika ushindi wa mabao 2-0 iliyopata juzi dhidi ya Mbao ya Mwanza.