Mchezaji nyota wa zamani wa Cameroon, Samuel Eto'o amewasilisha rasmi ombi lake la kugombea Urais wa Shirikisho la Soka nchini Cameroon siku ya Jumatano, na kuahidi kuwa yeye ndie Rais ajaye licha ya udanganyifu uliopangwa kufanyika.
Eto'o ambaye ameshawahi kushinda tuzo ya mchezaji Bora Afrika mara nne, alisindikizwa na umati mkubwa wa mashabiki wake wakati akiwasilisha nyaraka zake katika Makao Makuu ya Shirikisho la Soka Cameroon yaliyopo Yaounde.
“Nawatahadharisha wapinzani wetu wawe makini sana kwa kuwa tumeshapitia mambo mengi sana” Etoo ameviambia vyombo vya habari
Etoo mwenye umri wa miaka 40, na mchezaji wa zamani wa Barcelona na Inter Milan amesema uongozi wa sasa uliopo madarakani umemuahidi kumpa nafasi ya Makamu wa Rais endapo atajitoa katika kinyang'anyiro , jambo ambalo hajakubalianna nalo.
“mimi ndie Rais ajaye wa Shirikisho licha ya figisu zote zinazofanyika” ametanabaisha
Ni muda wa kufufua na kujenga mpira wetu, alisema Etoo wakati alipokua akiweka wazi nia yake ya kutangaza Urais mwezi Septemba
Uchaguzi wa Shirikisho la Mpira nchini Cameroon unatarajiwa kufanyika Disemba , mwezi mmoja kabla ya Cameroon kuendesha mashindano ya Mataifa Afrika (AFCON) michuano ambayo imechelewa kutokana na kuzuka kwa Janga la virusi vya Corona mwaka jana.