BEKI mkongwe wa timu ya taifa, Taifa Stars, Erasto Nyoni ameondolewa katika timu hiyo inayoshiriki Mashindano ya Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi za nyumbani (Chan) nchini Cameroon na kurejeshwa nchini.
Nyoni ndio mchezaji pekee wa Taifa Stars inayoshiriki mashindano Cameroon ambaye alikuwemo katika kikosi cha kocha Marcio Maximo kilichoshiriki Chan 2009 nchini Ivory Coast.
Taarifa ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) iliyotolewa jana ilisema kuwa, mchezaji huyo alirejeshwa nchini kutoka Cameroon baada ya ushauri wa jopo la madaktari ili aendelee na matibabu nchini. Hata hivyo, taarifa hiyo hakuweka wazi mchezaji huyo anasumbuliwa na nini.
Katika hatua nyingine, kikosi hicho kinaendelea kujiandaa na mchezo dhidi ya Guinea ambao wanahitaji ushindi ili kufuzu kwa robo fainali hizo wakati Namibia tayari imeshatolewa.
Namibia ilifungwa 1-0 na Stars baada ya kupokea kichapo kingine cha mabao 3-0 kutoka kwa Guinea na itakamilisha mchezo wake wa mwisho kwa kucheza dhidi ya Zambia iliyopo katika nafasi ya pili ikiwa na pointi nne sawa na Guinea.