Mabingwa watetezi wa Kombe la Dunia Timu ya Taifa ya Ufaransa imefuzu kwa hatua ya Nusu Fainali ya Michuano ya Kombe la Dunia inayoendelea nchini Qatar baada ya jana Desemba 10 kuichapa Timu ya Taifa ya England mabao 2-1.
Moto wa Ufaransa ni kama wanapingana na ile kauli iliyozuka miaka ya hivi karibuni kwa mabingwa watetezi kuboronga katika hatua za awali.
Ufaransa hilo kwao halipo kwani wameonesha kiwango bora tangu kuanza kwa michuano hii jambo linaloonesha wamedhamiria kulirudisha taji katika ardhi ya Ufaransa kwa mara ya pili.
Mabao ya Ufaransa yamewekwa kimiani na A. Tchouameni dakika ya 17 kipindi cha kwanza kabla ya Nahodha wa England Harry Kane kuisawazishia England kwa mkwaju wa Penati dakika ya 54.
Olivier Giroud akawarudisha Ufaransa katika uongozi baada ya kupachika bao dakika ya 78, na kwa mara nyingine Harry Kane akashindwa kuwasawazishia England baada ya kukosa mkwaju wa penati dakika ya 84.
Mpaka dakika ya 90 inakamilika Ufaransa wanaibuka na ushindi wa mabao 2-1, na kujikatia tiketi ya hatua ya Nusu Fainali ambao wanakwenda kukutana na Wawakilishi wa bara la Afrika timu ya Morocco.