Mchambuzi wa masuala ya soka nchini, Edo Kumwembe ameeleza kuwa aluyekuwa mshambuliaji wa Yanga SC, Fiston Kalala Mayele raia wa Congo DR ni zaidi ya Amisi Tambwe na Meddie Kagere.
Kupitia kipindi cha Sports Arena cha Wasafi FM, Edo amesema Mayele ambaye amesajiliwa na Pyramids FC ya nchini Misri licha ya kucheza miaka miwili pekee nchini Tanzania lakini uwezo wake umedhihirika kuwa ni wa juu zaidi kuliko Kagere aliyekiwasha Simba kwa miaka minne ambaye amecheza Simba na Yanga kwa miaka kadhaa tangu mwaka 2013.
"Mayele ameacha alama katika soka letu. Ameondoka akiwa ameuzwa bei ghali. Bei ambayo hakuna mchezaji wa soka la Tanzania amewahi kuuzwa. Inasemekana ni dola milioni 1, ni zaidi ya Tsh2.4 bilioni, pesa yetu ya madafu haina thamani.
"Achana na alama ya pesa ambayo ameacha, kitu cha msingi zaidi ni alama ya mabao aliyofunga. Mayele hajafunga mabao mengi zaidi ya Meddie Kagere au Amiss Tambwe katika soka letu. Labda wao wamecheza muda mrefu zaidi kuliko yeye.
"Kitu kikubwa ambacho ni aina yake ya mabao. Aliyafunga mabao kama mshambuliaji halisi zaidi kuliko hao wageni wengine. Alifunga mabao ambayo yalitustaajabisha kwa sababu alifunga katika mazingira magumu zaidi, ilikuwa nadra kwa Mayele kufunga mabao rahisi," amesema Edo Kumwembe.