Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Dodoma Jiji yatinga robo fainali FA

2756efc7fb100b8979856b3f4b83b714.jpeg Dodoma Jiji yatinga robo fainali FA

Sun, 2 May 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

TIMU ya soka ya Dodoma Jiji imefanikiwa kutinga robo fainali ya michuano ya Kombe la FA baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya KMC FC katika mchezo wa hatua ya 16 bora uliopigwa Uwanja wa Jamhuri Dodoma jana.

Matokeo hayo yanaifanya Dodoma Jiji kuungana na timu za Azam FC, Rhino Rangars, Mwadui FC, Yanga katika hatua ya michuano hiyo, ambayo mshindi anaiwakilisha Tanzania kwenye Kombe la Shirikisho Afrika (CAF).

Mabao yote mawili ya wenyeji Dodoma FC yalifungwa kipindi cha kwanza kupitia kwa washambuliaji, Seif Karie aliyefunga bao la kwanza dakika ya 19 akimalizia mpira uliopigwa na Khamis Mcha na kugonga nguzo na kurudi uwanjani kabla ya kukutana nao na kuumalizia wavuni.

Winga Dickson Ambundo alipoteza matumaini ya KMC kusonga mbele kwenye michuano hiyo baada ya kufunga bao la pili katika dakika ya 41, ikiwa ni baada ya yeye mwenyewe kufanya kazi nzuri ya kuwatoka walinzi wa wapinzani wao na kumalizia kirahisi.

KMC licha ya kuweka malengo makubwa kwenye michuano hiyo msimu huu, ilitengeneza nafasi moja ya kufunga katika kipindi cha kwanza, lakini mshambuliaji wake Matheo Anthon alikosa utulivu na kupaisha mpira juu.

Kipindi cha pili, KMC walirudi kwa kasi hasa baada ya kumtoa Matheo na kumuingiza Charles Ilamfya, ambapo waliweza kuutawala mchezo na kutengeneza nafasi nyingi za mabao, lakini walishindwa kuzitumia ipasavyo nakujikuta hadi dakika 90 za mchezo huo zinakamilika wako nyuma kwa mabao 2-0.

Chanzo: www.habarileo.co.tz