Mabosi wa Dodoma Jiji wapo mbioni kukamilisha usajili wa winga, Idd Kipagwile 'Mtoto Idd' aliyekuwa anacheza katika kikosi cha Polisi Tanzania.
Kipagwile ni mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake na Polisi Tanzania ambayo imeshuka daraja. Mabosi wa Dodoma Jiji ambao wapo jijini Dar es Salaam, tayari wameshamuita mchezaji huyo na kuanza kufanya mazungumzo kwa ajili ya kumpa mkataba wa miaka miwili.
Mtu wa karibu na mabosi wa timu hiyo, alilidokeza Mwanaspoti kwamba Kipagwile angeshamalizana nao mapema na timu hiyo lakini kuna baadhi ya makubaliano walikuwa bado hawajaafikiana.
"Kila kitu kimekaa sawa lakini mchezaji alikuwa na vitu ambavyo alitaka vibadilishwe kwenye mkataba wake, nadhani siku sio nyingi atasaini mkataba,"kilisema chanzo hicho.
Kipagwile anasifika kwa uwezo mkubwa wa kumiliki mpira na spidi pindi anapokuwa anapeleka mashambulizi langoni kwa timu pinzani.