Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Damas Ndumbaro wakati akizundua mashindano ya Silent Ocean Ramadhan Cup, amempongeza Rais wa TFF, Wallace Karia licha ya maneno mengi ya kukatisha tamaa yanayoelekezwa kwa Karia.
Dkt. Ndumbaro amesema maneno hayo yanatokana na kazi kubwa na nzuri anayoifanya Karia katika kuliongoza Shirikisho la Mpira wa Miguu [TFF].
“Najua Wallace Karia unapigwa vita sana, lakini mti wenye matunda ndio unapigwa mawe. Huwezi kuona mtu anapiga mawe kwenye mwarobaini, atakuwa na matatizo. Matunda yaliyopo kwenye mti huo ulioupanda ndio chanzo cha mawe unayoyapata.”
“Nakuahidi ushirikiano wa juu, sisi kama Serikali tunakuunga mkono kwa sababu TFF ndio chama cha mfano katika vyama vya michezo hapa Tanzania.”
Mbali na kumpongeza Karia, Dkt. Ndumbaro ameweka wazi kuhusu kipaumbele cha bajeti ya Serikali mwaka huu.
“Nichukue fursa hii kumshukuru Mh. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo amejitoa kuendeleza michezo hatimaye michezo inapata mafanikio kuliko kipindi chochote katika historia ya nchi.”
“Leo tunashuhudia Simba na Yanga zipo Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, haijawahi kutokea! Kwenye African All Games tumepeleka wachezaji wengi kuliko wakati wowote.”
“Katika bajeti ya Serikali ya mwaka huu kipaumbele namba moja ni michezo, maandalizi ya AFCON ndio kipaumbele namba moja kwenye bajeti ya mwaka huu.”