Kweli wana watu, ndicho unachoweza kusema kwa Wanajangwani Yanga katika dirisha hili la usajili baada ya mchana huu kushusha vifaa viwili katika jitihada za kujenga kikosi cha Mapambano kwa Ligi kuu na Ligi ya Mabingwa barani Afrika msimu ujao.
Mabingwa hao wa Kihistoria mchana huu wa Agosti 13, wametambulisha nyota wawili wa kigeni Djuma shabani na Jesus Moloko huku wachambuzi wa masuala ya soka wakidadavua kuwa, usajili wa Yanga safari hii unafanyika kitaalamu na kiufundi zaidi.
Usajili wote unaofanyika kwa sasa unafanyika kuboresha mapungufu yaliyojionesha msimu uliopita lakini pia kuziba nafasi zilizoachwa na nyota walioondoka klabuni hapo.
Tangu dirisha la Usajili kufunguliwa Klabu ya Yanga mpaka leo imekwishasajili nyota watano wa kimataifa.
Hivi karibuni Afisa Habari wa Yanga, Hassan Bumbuli alinukuliwa akisema nyota wao wote watakaosajiliwa msimu huu watakuepo kwenye safari ya kujiandaa na ligi nchini Morocco.
Hivyo basi kwa maana hiyo, siku ya Jumapili ambayo ndio kikosi cha Yanga kitaanza Safari, nyota hawa nao pia watasafiri na timu.