Waswahili wana msemo wao wenye busara wakikwambia usiku wa kulipa deni huwahi kukucha lakini sio usiku wa kwenda kung'oa jino.
Wakiwa na maana usiku ambao unakwenda kuleta mashaka katika siku yako kunawahi kupambazuka lakini sio ule usiku wa kwenda kutoa mashaka na tabu katika siku yako inayofuata.
Hayawi hayawi hatimaye yamekuwa. Leo ndio Disemba 11, siku iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu na wapenda kandanda wa nchi hii.
Siku ambayo vigogo wa Soka nchini Tanzania na Afrika Mashariki wanakwenda kuoneshana umwamba. Ni Simba dhidi ya Yanga.
Yanga ndio kinara wa Ligi mpaka hivi sasa akiwa na alama zake 19 kileleni mwa jedwali la msimamo wa Ligi, akifuatiwa na Mnyama mwenye alama 17 huku wote wakiwa wameshacheza michezo saba.
Hivyo ushindi wa leo kwa kila Timu ni muhimu sana. Lakini wakati wa kuelekea mpambano huu kuna vingi ambavyo vimejitokeza ikiwemo suala la Simba kugomea Mkutano wa Waandishi wa Habari kisa kuwepo kwa bango lenye Nembo ya GSM.
Bila shaka hata leo Uwanjani kutakua na nembo ya GSM katika maeneo mengi ya Uwanja, sasa swali la msingi je na leo watasusa? na kutunyima wapenzi wa Soka fursa ya kuburudika.
Majibu ya maswali yote haya yatapatikana saa 11:00 jioni pale kwa Mkapa Jijini Dar es Salaam.
Tusubiri Kipenga cha Mwamuzi aliepewa dhamana Heri Sasii, kitapulizwa kuashiria kuanza kwa mchezo, kitapulizwa kumaliza mchezo ama kitapulizwa kuahirisha mchezo ?