Klabu za Ligi Kuu England, Tottenham Hotspur na Aston Villa zipo kwenye vita kali ya kuwania saini ya kiungo wa Chelsea, Conor Gallagher katika dirisha hili la majira ya kiangazi.
Chelsea imeripotiwa kumweka sokoni kiungo huyo mwenye umri wa miaka 24, wakihitaji pesa kwa ajili ya mipango yao endelevu, kuelekea msimu ujao wa 2024/25.
Gazeti la The Mail limeeleza kuwa, Spurs iko tayari kushindana na Aston Villa katika mbio za kumsajili Gallagher na itafanya hivyo mwezi huu.
Spurs ina nia kubwa ya kumsajili mchezaji huyo wa kimataifa wa England, na wanajiandaa kutuma ofa huko Stamford Bridge kumnasa staa huyo, ambaye pia anawindwa na Atletico Madrid ya Hispania.
"Kwa kweli, Spurs ianahisi itapata fursa ya kupata mkataba mzuri wa thamani kwa Gallagher kabla ya Juni 30.” limeandika gazeti la The Mail
Awali Aston Villa ilitajwa pekee yake kuhitaji huduma ya Gallagher, lakini ushindani kutokakwa Spurs unaendelea kudhihirisha umuhimu wa kiungo huyo ambaye alipandishwa kwenye kikosi cha kwanza cha Chelsea mwaka 2019.
Gallagher amewahi kutolewa kwa mkopo katika klabu za Charlton Athletic (2019–2020), Swansea City (2020), West Bromwich Albion (2020–2021) na Crystal Palace 2021–2022.