Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Coastal Union yarudisha pesa za Simba usajili wa Lameck Lawi

Lameck Lawi Eliass Lameck Lawi

Fri, 21 Jun 2024 Chanzo: Mwanaspoti

Muda mchache baada ya Simba kumtambulisha beki wa kati wa Coastal Union, Lameck Lawi baada ya kumsajili kwa mkataba wa miaka mitatu, mapya yameibuka.

Ipo hivi. Mwanaspoti ndio lilikuwa gazeti la kwanza kuandika stori ya beki huyo kusaini mkataba wa miaka miwili kuitumikia Simba msimu ujao, lakini mambo yameenda tofauti.

Chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya Coastal kimeliambia Mwanaspoti kuwa, Lawi sio mchezaji wa Simba kama ilivyomtangaza huku kikiweka wazi Wekundu wa Msimbazi hao wamemkosa staa huyo kutokana na kuchelewesha malipo.

“Simba ni kweli walikuja mezani kufanya mazungumzo ya kumsainisha Lawi na makubaliano yalienda vizuri kwa kukubaliana timu hiyo kulipa fedha za usajili muda ambao tulikubaliana, lakini hawakufanya hivyo,” kilisema chanzo hicho na kuongeza;

“Tumerudisha fedha ya Simba ambayo imeingia tofauti na makubaliano tunashangazwa na timu hiyo kuamua kutangaza mchezaji wetu kuwa ni wao hili sio sawa.”

Mwanaspoti awali liliripoti kuwa beki huyo wa kati alikubaliana na Simba kusaini mkataba wa miaka miwili wenye thamani ya Sh 205 Milioni japo jana Simba ilitangaza kumpa miaka mitatu akiwa mchezaji wa kwanza kutangazwa tangu dirisha la usajili lifunguliwe Juni 15.

Beki huyo ambaye ni panga pangua kikosi cha kwanza cha Coastal ameisaidia timu hiyo kuwa katika nafasi ya nne ya msimamo wa Ligi Kuu Bara baada ya kucheza mechi 25 na kufanikiwa kukusanya pointi 34 na kukata tiketi ya kucheza michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Pia Coastal ilifika hatua ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho (FA) na kufungwa na Azam FC kwa mabao 3-0.

Viongozi wa Simba hawakupatikana kutoa ufafanuzi wa madai hayo ya Coastal Union.

Chanzo: Mwanaspoti