Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Chuma kipya chanukia Simba, ni mwamba kweli

Elie Mpanzu Winga wa kulia kutoka AS Vita ya Jamhuri ya Kidemkorasi ya Congo (DRC), Elie Mpanzu.

Sat, 1 Jun 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Kazi iendelee, uongozi wa Wekundu wa Msimbazi umetajwa uko katika hatua za mwisho za kumsajili winga wa kulia kutoka AS Vita ya Jamhuri ya Kidemkorasi ya Congo (DRC), Elie Mpanzu, imeelezwa.

Habari za ndani zinasema mazungumzo kati ya Simba na Mpanzu yanaendelea vyema na baadhi ya makubaliano kati ya winga na klabu hiyo yameshafanyika ili mchezaji huyo aje kuichezea timu yake mpya.

Chanzo chetu kiliendelea kusema Simba imedhamiria kuboresha kikosi chake baada ya kutokuwa na matokeo mazuri katika msimu uliopita ambapo ilimaliza kwenye nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara na pia ikiishia hatua ya robo fainali ya mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

"Ni kweli huyu mchezaji tumezungumza naye na mambo yanakwenda vizuri, ambacho watu hawaelewi ni alikuwa chaguo letu hata msimu uliopita lakini tulimkosa, msimu huu tumekwenda na dhamira moja kwa sababu tunataka kufanya maboresho makubwa kwenye kikosi chetu, mambo yanakwenda vizuri vimebaki vitu vichache tu ili kumalizana," kilisema chanzo chetu.

Kiliongeza benchi la ufundi la Simba linaamini usajili wa mchezaji huyo mwenye miaka 22, ambaye amepachika mabao 11 kwenye Ligi Kuu ya DRC msimu huu ukikamilika, utakuwa usajili wa kwanza wa klabu hiyo kwa wachezaji wa kigeni.

Chanzo hicho kilisema pia Simba inatajwa kumwania, Derrick Fordjour, kutoka Medeama ya Ghana pamoja na straika wa Red Arrows ya Zambia, Ricky Banda.

"Kuna Banda (Ricky), mwingine huenda akatua Simba msimu ujao, ni moja ya wachezaji waliofanya vyema katika Ligi ya Zambia msimu huu unaomalizika, mazungumzo yanaenda vyema na anaweza kumwaga wino wakati wowte," kilisema chanzo hicho.

Taarifa zaidi zinasema katika kuunda kikosi imara na chenye ushindani zaidi, huenda klabu hiyo ikaachana na baadhi ya wachezaji wake akiwamo Mrundi Saido Ntibazonkiza, Luis Miquissone, Mgambia Jobe Pa Omar, Freddy Michael, Babacar Sarr na Mkongomani Henock Inonga.

"Bado kuna wingu katika usajili wa Aishi Manula, kuna mambo mengi yanaendelea, kubakia au kuondoka Simba iko mikononi kwake mchezaji, atakavyoamua, kama fedha anazotaka atapewa.

Hilo ni panga la awamu ya kwanza, pia kuna panga lingine ambalo litawahusisha zaidi wachezaji wazawa, lengo ni kusajili nyota wengine wenye viwango vya juu ili kuirudisha timu hiyo kwenye makali yake yaliyozoeleka," kiliongeza chanzo chetu.

Meneja Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally, alisema ni kweli kikosi chao kinahitaji marekebisho makubwa kwa ajili ya kurejesha heshima.

Ahmed amewataka wanachama na mashabiki wa Simba kutulia wakati huu ambao viongozi wao 'wanahaha' kuandaa kikosi 'tishio' cha msimu ujao.

"Tunajua kipindi hiki mambo yatakuwa mengi na tutasikia taarifa nyingi za usajili, Simba tutafanya usajili mkubwa sana safari hii, ila ni nani, anatoka wapi, na majina yao, tutautangaza pale tutakapoona inafaa kupitia vyombo vyetu," Ahmed alisema.

Simba imemaliza Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2023/2024 katika nafasi ya tatu, nyuma ya mabingwa, Yanga na Azam FC zote za Dar es Salaam.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live