Nyota wa Azam FC, Shaban Chilunda ataukosa mchezo wa kesho Januari 6 dhidi ya Namungo FC baada ya kuumia katika mchezo wa jana.
Jana Azam ilicheza na Meli 4 City na kushinda bao 1-0 bao ambalo lilifungwa na Chilunda kwenye Uwanja wa Amaan ikiwa ni hatua ya makundi ya mashindano ya Kombe la Mapinduzi.
Akizungumza na Mwanaspoti, Chilunda alisema pamoja na kukosekana kwake ila anaamini timu yake itashinda kauli iliyoungwa na mshambuliaji mpya Ibrahim Ajibu.
Nyota hao wamesema Namungo ni timu nzuri na tayari imeshinda mechi mbili na kuwa na uhakika wakucheza nusu fainali hivyo wanapaswa kuwa makini kuhakikisha wanashinda mechi hiyo.
"Nasikitika kuikosa hiyo mechi na nitakuwa nje ya uwanja kama wiki moja hivi kutokana na kuumia jana ila naamini watakaocheza watafanya vizuri ingawa mechi haitakuwa rahisi," amesema Chilunda
Kwa upande wa Ajibu amesema kuwa; "Hatupaswi kuidharau Namungo ni timu ngumu na ninaifahamu hivyo mechi ya kesho itakuwa na upinzani mkubwa, tutaingia uwanjani tukihitaji ushindi na ndiyo lengo letu kubwa,"
Chilunda amerudi kwenye timu yake ya zamani baada ya kuvunja mkataba na timu ya Tenerrif ya Hispania.