Mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Tanzania Bara umekamilika jana Disemba 7 kwa michezo miwili ambapo Yanga wamemaliza kibabe wakiichapa Namungo huku Coastal wakiiduwaza Singida kwa kipigo cha magoli 2-1.
Wapo mastaa ambao wamefanya mambo mazito katika mzunguko huu ambao mpaka makala hii inatengenezwa vinara wa msimamo wa Ligi Kuu Bara walikuwa Yanga pale juu na wafuatao ni mastaa wa kigeni ambao wanaunda kikosi cha kwanza kwa wachezaji wa kigeni kulingana na takwimu zao viwanjani
Djigui Diarra
Kipa namba moja wa Yanga ambaye mpinzani wake ni mzawa yule wa Simba, Aishi Manula, Diara msimu huu ameshacheza mechi 11 mpaka sasa sawa na dakika 990 uwanjani. Takwimu zake bora zingine ni kuwa na sevu 13 pia akiokoa penalti 1.
Nicholas Gyan
Akiwa na klabu yake ya Singida Big Stars amekuwa akitumika kama beki wa kulia na hata winga wa kulia. Mpaka sasa amefanikiwa kutengeneza asisti 4 kwenye ligi akimzidi beki mwingine wa kulia Nicholas Wadada wa Ihefu aliyetengeneza asisti moja na bao 1 katika michezo 9 aliyocheza sawa na dakika 772.
Bruce Kangwa
Beki wa kushoto wa Azam ataendelea na jukumu hilo kwenye kikosi hiki kutokana na kazi bora yake Azam Complex, akicheza michezo 10, sawa na dakika 810 ingawa hana bao wala asisti.
Henock Inonga
Beki wa kati wa Simba ambaye ameendelea na kuwa na wakati mzuri katika michezo 14 aliyocheza sawa na dakika 1260 akikosa mechi moja tu baada ya kuugua kabla ya mchezo kuanza.
Joash Onyango
Kando na Inonga mtu ambaye anamuongezea ubora Mkongomani huyo ni Mkenya huyu ambaye msimu huu alirejea na nguvu akiutihibitishia uma wa klabu yake kwamba bado anastahili kuvaa jezi za wekundu hao akicheza michezo 12 sawa na dakika 990.
Khalid Aucho
Kiungo mkabaji wa Yanga ambaye amekuwa mhimili mkubwa kwa timu yake ndani ya miaka miwili hii, msimu huu amecheza michezo 12 sawa na dakika 812 alizokuwa uwanjani lakini ukiacha ukabaji wake pia ametoa asisti 2.
Yannick Bangala
Pembeni yas Aucho mashabiki wa Yanga wanafurahia kupenda kumuona huyu ambaye alikuwa mchezaji bora wa msimu uliopita, akicheza mechi 11 sawa na dakika 911 akiwa na bao moja tayari.
James Akamiko
Kiungo fundi wa Azam anayecheza msimu wa kwanza hapa nchini lakini akianza katika kiwango bora, akicheza michezo 13 sawa na dakika 950 akiwa na bao 1 na asisti 2
Fiston Mayele
Mshambuliaji wa Yanga anayeongoza kwa ufungaji katika ligi akiwa amefunga mabao 10 akiwa na asisti 1 akicheza michezo 12 sawa na dakika 897.
Mosses Phiri
Pembeni ya Mayele atacheza mshambuliaji huyu wa Simba ambaye ameendelea kuwa na moto katika msimu wake wa kwanza hapa nchini naye akifunga mabao 10, akimzidi asisti moja Mkongomani huyo katika michezo 15 aliyocheza sawa na dakika 1275.
Clatous Chama
Kiungo fundi wa Simba huyu ambaye amekuwa na moto mkali msimu huu na hakuna aliye bora kwa wageni kwa nafasi yake kumzidi mkapa sasa akicheza michezo 12 sawa na dakika 1057 akikosa mechi tatu kutokana na kusimamishwa michezo 3, akifunga mabao 2 huku akitoa asisti 7, akimzidi Ayoub Lyanga kwa asisti moja pekee.
Sub
Kwenye wachezaji wa akiba kanuni inataka timu kuwa na wachezaji wasiopungua 7 ambapo mastaa hawa wanaweza kuwa hapa wakisubiri kucheza katika kikosi cha kwanza.
Arakaza MC Artur,
Nico Wadada,
Biemes Carno,
Moubarack Amza,
Jesus Moloko,
Idris Mbombo na
Sadio Kanoute
KOCHA NASREDDINE NABI
Kocha huyu wa Yanga atakuwa na kikosi hiki achana na kutofungwa mechi 49, lakini msimu huu amepoteza mechi moja iliyositisha rekodi hiyo ngumu na pia akiwa tayari na tuzo moja ya kocha bora huku pia timu yake ikiongoza ligi.