Kuelekea msimu ujao, Bodi ya Ligi Tanzania Bara (TPLB), imetangaza kubadilisha majina ya Ligi Daraja la Kwanza na Daraja la Pili.
TPBL imeeleza kuwa kuanzia msimu mpya wa 2021/2022, iliyokuwa Ligi Daraja la Kwanza (FDL), ambayo inafuata kwa ukubwa baada ya Ligi Kuu, itaitwa Championship na ile Daraja la Pili (SDL) itaitwa First League.
Sambamba na hilo, huenda msimu ujao Ligi Daraja la Kwanza (Championship) ikachezwa kama ligi ya kawaida tofauti na misimu iliyopita ilivyokuwa ikichezwa kwa makundi mawili.
Akizungumza na Mwanaspoti, Ofisa Habari wa TPLB, Karim Boimanda amesema kuwa marekebisho mengine ya ligi hizo yamekamilika na muda wowote kuanzia leo yatatangazwa kwa Umma.
"Ili kuendana na mabadiliko na maendeleo ya soka duniani, kuna marekebisho yamefanyika ambayo ni tofauti na ilivyokuwa awali na tutatangaza siku chache zijazo," amesema Karim.
Timu zitakazoshiriki Championship ni Mwadui, JKT Tanzania, Ihefu, DTB, Pan African, Green Warriors, Mashujaa, African Sports, Ken Gold, Ndanda, Kitayosce, Fountain Gate, African Lyon, Pamba na Transit Camp.