Nahodha wa Timu ya Simba John Bocco amefunguka kuwa mchezo wao wa Pili wa hatua ya Makundi Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Union Sportive Gendarmerie Nationale utakuwa mgumu kuliko wengi wanavyodhani.
Bocco ameyasema hayo leo Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA) muda mfupi kabla ya kuanza safari ya kuelekea nchini Niger ambapo kutapigwa mchezo huo Jumapili saa moja usiku.
Bocco amesema licha ya US Gendarmerie kupoteza mchezo wake wa kwanza dhidi ya RS Berkane haimaanishi ni timu mbovu hivyo wataingia kwa tahadhari kubwa.
"Hatua hii tuliyofikia hakuna mechi rahisi. Gendarmarie imetoka kupoteza mchezo uliopita ugenini hivyo hawatakubali kufanya hivyo tena wakiwa nyumbani"
"Tunaondoka vichwani mwetu tunajua tunaenda kukutana na upinzani mkubwa lakini tumejiandaa kuhakikisha tunapata matokeo mazuri" amesisitiza Bocco