TIMU ya Biashara United imetoa ofa kwa mashabiki 100 wa kwanza watakaopata chanjo ya Uviko-19, kuingia uwanjani bure kuangalia mechi yao dhidi ya Simba.
Kwa mujibu wa uongozi wa Biashara United, wameamua kufanya hivyo wakishirikiana na uongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Musoma ili kuhamasisha watu kupata chanjo ya Uviko-19.
Mrwenyekiti wa Biashara United, Seleman Mataso ameeleza kuwa wameamua kufanya hivyo ili kuendeleza nia yao ya kuisaidia jamii inayowazunguka.
“Watu 100 watakaochanja mapema wataingia uwanjani bure, na kama unavyoona tumeweka matangazo na gari kubwa la matangazo linapita likihamasisha watu kujitokeza uwanjani kuchanja,” amesema Mataso na kuongeza;
“Biashara ni timu ya Jamii hivyo lazima kila linaloihusu jamii tuhusike nalo, pia mashabiki wetu wajitokeze kwa wingi kupima na kuingia uwanjani kuishangilia timu hii kwani tumejipanga kuwafurahisha leo,” amesema Mataso.
Mechi kati ya Biashara na Simba inatarajiwa kuanza Saa 10:00 jioni kwenye Dimba la Karume mjini Musoma.