Wanajeshi wa Mpakani, timu ya Biashara United ambayo inashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika, inacheza mchezo wake wa raundi ya kwanza Oktoba 15 dhidi ya Al Ahly Tripoli, Majira ya saa 9:00 Alasiri katika uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
Lakini Hofu ya walio wengi ni kuona mchezo wa Marudiano baina ya timu hizo ukipangwa kufanyika nchini Libya kwa kuwa hali ya kiusalama sio shwari nchini humo
Sasa Meneja wa Biashara United Frank Wabare amezungumza kuhusiana na changamoto hiyo;
"Unajua hata sisi tulijua huu mchezo utapelekwa nchi nyingine kama Morocco au Misri, lakini tumeshangaa umeamuliwa na CAF uchezwe Libya, sisi tuko tayari na tumeshajipanga kwenda popote pale"
"CAF wao ndio wenye mashindano na mpaka wameamua hivi basi bila shaka wamejiridhisha na hali ya usalama, wapenzi na mashabiki wetu wasitie shaka sisi ndio wanajeshi wa mapakani na tunakwenda kuonesha uhalisia wa jina letu" amesema Wabare
Mchezo wa Marudiano baina ya Al Ahly Tripoli dhidi ya Biashara United utapigwa Oktoba 22-25 nchini Libya.