Timu ya Biashara United imeanza rasmi mazoezi katika uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam kwa ajili ya mchezo wa Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) dhidi ya Yanga unaotarajiwa kupigwa Februari 15.
Timu hizo zinakutana kwenye hatua ya 16, bora mchezo utakaopigwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Timu ya Mwanaspoti leo ilikuwa uwanjani kushuhudia timu hiyo inayonolewa na Bahati Vivier wakifanya zaidi mazoezi ya mbinu.
Vivier aliwataka wachezaji wake wacheze mpira wa chini na utulivu huku zoezi hilo likionekana kueleweka.
Wachezaji hao walikuwa wanacheza bila kuwa na goli la kufunga hali ambayo iliwafanya muda wote kuufuata mpira.
Yanga ilifuzu hatua hiyo baada ya kuiondosha Mbao FC kwa bao 1-0 kwenye hatua ya 32, huku Biashara United ikitinga hatua hii kufuatia kuiondosha Mbeya Kwanza mabao 2-1.
Hii ni mara ya pili kwa timu hizo kukutana msimu huu baada ya awali kukutana kwenye Ligi Kuu Bara Decemba 26, 2021 ambapo Yanga iliibuka na ushindi wa mabao 2-1.