Mkongwe wa soka David Beckham amevunja ukimya na kutetea uamuzi wake wa kukubali kuwa Balozi wa Kombe la Dunia Qatar 2022, dili nono lililosababisha akosolewe vikali.
Akizungumza na tovuti ya The Telegraph Nyota huyo wa zamani wa England amesema ”Huwa nafanya utafiti kwa washirika ambao naenda kufanya nao biashara, na nilitaka kuwa sehemu ya Kombe la Dunia"
"Napenda kuiona soka ikikuwa na hiyo ina maana kuwa soka inabidi iende maeneo ambayo haijawahi kwenda kabla”
”Nilijua yatakuwepo maswali, nitakosolewa, hata hivyo siku zote nimekuwa nikiamini kuwa soka ni chombo chenye nguvu”
”Nilikaa kule mwezi mzima, na hakuna mtu hata mmoja aliyenifuata na kusema ”Ooh nimetendewa hivi, Ooh nimetengwa, sikukubaliwa kuingia hapa au pale. Hivyo, uamuzi wangu wa kufanya kazi na Qatar niliufurahia."
Beckham ana mkataba wa miaka 10 kama Balozi wa Qatar. Mkataba huo ambao utahusu kuitangaza nchi unadaiwa kumlipa takribani Pauni milioni 125.