Winga wa zamani wa Manchester United, David Beckham amemfuta kazi mchezaji mwenzake wa zamani wa Mashetani wekundu, Phil Neville kama kocha mkuu wa klabu ya Inter Miami huku Javier Morales akipewa jukumu la kuwa kocha wa muda wa klabu hiyo inayoshiriki Ligi kuu ya MLS Marekani.
Beckham ambaye ni mmiliki mwenza wa klabu hiyo amepitisha shoka hilo baada ya ghadhabu kutoka kwa mashabiki kufuatia kipigo cha 1-0 dhidi ya New York Red Bulls kinachoiweka klabu hiyo mkiani mwa msimamo wa Ligi ya MLS Eastern Conference.
Mashabiki walionesha mabango ya kutaka Neville atimuliwe kufuatia kipigo hicho ambapo pia walimzomea mtoto wa kocha huyo, Harvey Neville ambaye anachezea klabu hiyo.
Neville (46) alipewa jukumu la kuinoa klabu hiyo mnamo Januari 2021 lakini msimu huu umekuwa na matokeo mabaya huku klabu hiyo ikiambulia alama 15 katika mechi 13, ushindi mara 5 na vipigo 8.