Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Innocent Bashungwa, amesema wanajipanga kimkakati kwa kushirikiana na wizara ya utamaduni ili kuona namna bora ya kutambua na kuviendeleza vipaji vya michezo jeshini.
Bashungwa ameyazungumza hayo leo Julai 10, 2023 kwenye maadhimisho ya miaka 60 ya Jeshi la Kujenga Taifa yaliyofanyika katika Uwanja wa Jamhuri Dodoma.
"Tunajipanga kuweka mazingira sahihi ya kutambua vipaji ili kuboresha mafanikio ambayo mwaka huu tumeyapata katika jeshi letu ambapo tumeona timu zetu za Mashujaa na JKT Tanzania zimefuzu kucheza Ligi Kuu ya NBC msimu ujao," alisema Bashungwa akibainisha mikakati ya wizara hiyo kuendelea kuibua vipaji vya kimichezo kama walivyofanya kwa timu za JKT Tanzania, Mashujaa FC, JKT Queens na walivyoibua wanamasumbwi mbalimbali nchini.