BEKI wa timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ na Baroka ya Afrika Kusini, Abdi Banda amesema hawajaenda kwenye fainali za Mataifa ya Afrika nchini Misri kama watalii.
Kikosi cha Stars kiliondoka jana kwenda Misri kikiwa na wachezaji 32 ambapo wataweka kambi ya wiki mbili kabla ya kuanza fainali hizo, Juni 21 mwaka huu.
Banda alisema pamoja na ugumu wa kundi C walilopangwa na timu za Algeria, Senegal na Kenya wana nafasi ya kupambana na kuvuka hatua hiyo.
“Sioni kama inashindikana kuvuka hatua ya makundi, tumekuja kushindana na sio kushiriki ndio maana napata ujasiri wa kusema hivyo.
“Kuna kitu cha tofauti nakiona kwenye timu, kila mchezaji anaonekana kuwa na shauku ya kutaka kuonyesha kuwa sisi sio wanyonge kwenye kundi letu,” anasema Banda.
Msimu uliopita wa 2018/19, Banda akiwa na Baroka amefunga bao moja kwenye michezo 13 ya Ligi Kuu Afrika Kusini ambayo ni maarufu kama PSL.