Mabeki wa Kikosi cha Yanga, Ibrahim Hamad Bacca na Bakari Nondo Mwamnyeto, wamerejea mazoezini baada ya kukosekana kwa muda kutokana na kusumbuliwa na majeraha.
Nyota hao walirejea kambini wakitokea kwenye majukumu ya Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars iliyokwenda kushiriki michuano ya AFCON nchini Ivory Coast wakiwa majeruhi.
Bacca alikuwa akisumbuliwa na majeraha ya enka, wakati Mwamnyeto tatizo lake likiwa ni jeraha la paja, lakini sasa wote wamepona.
Kurejea kwa nyota hao mazoezini, kunafanya kupunguza idadi ya majeruhi kikosini na kuimarisha timu kuelekea michezo ijayo ya Ligi Kuu ya NBC na Ligi ya Mabingwa Afrika.