Baada ya kujihakikishia nafasi kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao, klabu ya Azam imeendelea kujiimarisha baada ya kutangaza kukamilisha uhamisho wa mshambuliaji Jhonier Blanco raia wa Colombia kutoka klabu ya Aguilas Doradas ya mji wa Rionegro, inayoshiriki Ligi Kuu ya Colombia.
Blanco aliyezaliwa Oktoba 18, 2000, amesaini mkataba wa miaka minne baada ya kufaulu vipimo vya afya, kufuatia makubaliano baina ya klabu yake na Azam FC.
Taarifa ya Azam FC imeeleza kuwa nyota huyo alianzia soka lake kwenye akademi ya Club Deportivo Estudiantil kabla ya kujiunga na timu ya ligi kuu ya Aguilas Doradas na kutolewa kwa mkopo kwenye klabu ya daraja la kwanza ya Fortaleza.
Akiwa na klabu hiyo aliibuka kuwa mfungaji bora na kuisaidia kupanda daraja. Baada ya mkopo akarudi klabuni kwake Aguilas Doradas hadi sasa ambapo Azam FC imemnunua.