Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Aziz Ki, Diarra kuifilisi Yanga

Aziz Diarra 0002 Aziz Ki na Diarra

Sat, 15 Jun 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wakati dirisha la usajili wa wachezaji limefunguliwa rasmi leo, uongozi wa mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga unasisitiza nyota wake, Stephano Aziz Ki na kipa chaguo la kwanza, Djigui Diarra, wataendelea kubakia katika kikosi chao, imeelezwa.

Nyota mwingine ambaye Yanga inakaribia kumbakiza ili kupata huduma yake ni Pacome Zouzoua.

Nyota hao watatu wamemaliza mkataba wa kuwatumikia Yanga, na mabosi wanaendelea kukamilisha mazungumzo ili watie saini mikataba mipya, huku kukiwa na tetesi wanawindwa na vigogo mbalimbali wa ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumza nasi jana, Ofisa Habari wa Yanga, Ali Kamwe, alisema klabu hiyo itatumia kila rasilimali yake ili kuhakikisha inawabakisha wachezaji nyota wote walioipa mafanikio timu yao kwenye msimu uliopita.

Kamwe alisema pia mabosi wa klabu hiyo wako katika hatua za mwisho za kusajili nyota wapya ili kukiongezea nguvu kikosi chao kuelekea msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara na mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Ofisa huyo amewataka wanachama na mashabiki wa Yanga kutokuwa na wasiwasi wa kuondokewa na nyota wao na waelewe kipindi hiki huongozwa na propaganda.

"Wanachama na mashabiki wa Yanga wamekuwa na furaha na amani kwa kipindi chote cha msimu, hivyo wasikae kwa kusononeka kipindi hiki kutokana na yanayosemwa watapoteza baadhi ya wachezaji wao nyota," alisema Kamwe.

Aliongeza tayari wameshaanza kuifanyia kazi ripoti ya benchi la ufundi lililoko chini ya Kocha Mkuu, Miguel Gamondi na watampa kila kitu ambacho ameelekeza kwa sababu wanataka kufikia malengo.

"Kwa sasa tunaifanyia kazi ripoti ya benchi la ufundi juu ya kukiboresha kikosi chetu, kwanza kabisa kila mchezaji wanamhitaji abaki kikosini, atabaki, uongozi utafanya hivyo, kwa hiyo wanachama na mashabiki wetu hawatakiwi kuwa na wasiwasi wowote, atakayeondoka ujue hahitajiki.

Kila aliyeifanya timu kuwa tishio msimu uliopita tutatumia nguvu zetu zote tulizonazo kumbakisha, tunataka kutengeneza timu tishio zaidi msimu ujao kuliko hii iliyopita," Kamwe alisema.

Aliongeza Yanga inafanya mchakato wa usjaili kwa umakini mkubwa na haufanyiki kwa kufuata na mihemko.

"Tutamsajili mchezaji yoyote tunayemhitaji, niwaambie mashabiki na wanachama wa Yanga, uongozi wao uko makini katika usajili, na hatuingizwi mkenge na baadhi ya wachambuzi, tutakachofanya ni kusajili wachezaji ambao watakiongezea thamani na ubora kikosi tulichokuwa nacho," alisema ofisa huyo.

Hata hivyo, Kamwe alisema Yanga bado haijaamua kama itashiriki mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati maarufu Kombe la Kagame ambayo yanatarajiwa kufanyika kuanzia Julai 6 hadi 22, mwaka huu hapa nchini.

Tayari Azam imeshatangaza kujitoa kushiriki michuano hiyo inayoandaliwa na Baraza la Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), huku wawakilishi wengine kutoka Bara wakiwa ni Simba na Coastal Union.

"Bado hatujafikia uamuzi, kila kitu kitawekwa hadharani tutakapofikia uamuzi," alisema kwa kifupi Kamwe.

Habari zilizopatikana jijini zinasema mbali na kumtaka kwa udi na uvumba, straika, Prince Dube, ambaye bado ana magogoro wa kimkataba na waajiri wake, Azam FC, Yanga ipo mbioni kumalizana na Charve Onoya, kiungo mkabaji na kiungo mshambuliaji, Agee Basiala, wanaokipiga katika klabu ya AS Maniema ya Jamhuri ya Kidemkorasi ya Congo (DRC).

Mabingwa hao wa Kombe la FA wanatajwa pia wanakaribia kumalizana na beki wa kati, Chadrack Boka kutoka Saint Eloi Lupopo ya DRC.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live