Kiungo wetu, Stephane Aziz Ki amemaliza utata baada ya kuwepo kwa tetesi nyingi zilizomuhusisha kuwa mbioni kuondoka huku mwenyewe akisema hilo haliwezi kutokea kama hajatimiza malengo yake.
Aziz Ki huu ni msimu wake wa pili ndani ya Young Africans, amekuwa na wakati mzuri akiisaidia timu kubeba mataji mawili mfululizo ya Ligi Kuu ya NBC na kucheza fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika msimu wa 2022-2023.
Nyota huyo raia wa Burkina Faso, katika sherehe za ubingwa juzi Uwanja wa Benjamin Mkapa, alianika wazi kila kitu.
Rais wa Young Africans, Eng. Hersi Said, ndiye aliyefichua jambo hilo ambapo alizungumza na Wananchi akiwa sambamba na Aziz Ki akisema mwamba huyo haondoki.
“Aziz Ki amesema haondoki ndani ya Yanga mpaka afanikishe malengo yake, hivyo ataendelea kuwepo,” alisema Eng. Hersi.