Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Stephanie Aziz KI ambaye ni mfungaji bora wa Ligi Kuu amefunguka kuhusu bao lake bora msimu huu akitaja kuwa ni lile alilofunga dhidi ya Azam FC kwenye duru la kwanza la ligi.
Katika mchezo huo, Yanga waliibuka na ushindi wa mabao 3-2 huku Aziz KI akifunga mabao yote matatu licha ya kutanguliwa mabao 2-1 na Azam na kuisaidia timu kuibuka na ushindi.
“Kwangu mimi ni hat-trick niliyofunga dhidi ya Azam kwa sababu nilifunga bao la kwanza wakafunga na wao, kisha wakafunga tena na mwisho wa siku tukarudisha na nikafunga bao la ushindi dakika za mwisho kabisa, kwa hiyo lilikuwa jambo mhimu timu ipate ushindi.
“Jana (juzi) timu ilishinda mabao 4-1, najua nilifunga hat-trick lakini jambo kubwa lilikuwa timu ishinde kwanza haijalishi nani anafunga.
“Bao langu bora ni lile nililofunga la mwisho dhidi ya Azam Fc kwenye mzunguko wa kwanza kwa sababu timu ilikuwa chini sana baada ya Azam FC kufunga bao la pili, na mimi nikaja kufunga bao na kuisaidia timu yangu kupata ushindi dakika za majeruhi kabisa,” amesema Aziz KI.